TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA TAASISI YA KWANZA KUMPUNGUZIA MWANANCHI GHARAMA ZA USAILI


Na Jeremia Lubango na Lydia Churi-Dodoma, Dar es salaam

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel amesema Tume ya Utumishi wa Mahakama imekuwa ni Taasisi ya kwanza kumpunguzia mwananchi gharama katika suala la upatikanaji wa ajira nchini.

Akizungumza na Waandishi wa Habari wakati wa Usaili wa Watumishi wa Mahakama uliofanyika jana katika maeneo mbalimbali nchini akiwa katika kituo Jumuishi cha Utoajhi haki jijini Dodoma, Prof. Ole Gabriel amesema Tume imekuwa ni  Taasisi ya kwanza kubuni utaratibu wa kutumia TEHAMA katika usaili wa awali yaani kabla ya Msailiwa kufika kwenye hatua ya mahojiano ya ana kwa ana (Oral Interview).

“Matumizi ya mfumo wa Kielektroniki yameiwezesha Tume kufanya Usaili kwa wakati moja katika maeneo mbalimbali nchini na hivyo kumpunguzia gharama anayefanya Usaili ambapo sasa hatalazimika kusafiri kutoka eneo moja kwenye lingine kwa ajili ya kufanya usaili”, alisema Katibu huyo wa Tume.

Alisema tangu mwaka 2022, Tume iliona kuna umuhimu wa kutumia mfumo wa kielektroniki katika mchakato wa ajira za Watumishi wa Mahakama kwa lengo la kupunguza gharama, kuleta uwazi zaidi na kupunguza malalamiko kwa baadhi ya waombaji wa nafasi za kazi zinazotangazwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Katibu wa Tume alisema mwaka huo, Tume kwa kushirikiana na Wataalam wa TEHAMA kutoka Mahakama ya Tanzania ilibuni na kusanifu Mfumo wa maombi ya kazi “ JSC Recruitment portal” ili kufanikisha mchakato wa ajira za watumishi wa Mahakama ya Tanzania.

“Mwaka 2022, Mfumo ulianza kutumika kwa majaribio na kuonesha mafanikio  yakiwemo kupunguza malalamiko kwa baadhi ya waombaji wa nafasi za kazi kazi, kupunguza muda wa mchakato wa ajira hadi kufikia siku 45 Kutoka siku 90 za mfumo wa awali, kurahisisha uchambuaji wa taarifa, Kuboresha Utendaji kazi  na kuwapunguzia gharama waombaji wa kazi kwa kufanya usaili mahali walipo au karibu na maeneo yao”, alisema.

Aliyataja maeneo ambapo usaili huo ulifanyika jana kuwa ni Arusha, Mwanza, Dar es salaam, Tanga, Moshi, Kigoma, Iringa, Dodoma, Tabora, Shinyanga, Songea, Sumbawanga, Morogoro, Mbeya, Musoma, Mtwara na Bukoba.  

Mamlaka ya Tume ya Utumishi wa Mahakama kama chombo cha kusimamia ajira na nidhamu za watumishi wa Mahakama yanatokana na Ibara ya 113 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Toleo la mwaka 1977 ikisomwa pamoja na Kifungu Na. 29 (1) cha Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Na. 4 ya mwaka 2011.