KAMISHNA WA TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA AMTEMBELEA KATIBU WA TUME OFISINI KWAKE DODOMA
Na Stanslaus Makendi-Mahakama Kuu, Dodoma
Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania ambaye pia ni Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Dkt Gerald Ndika hivi karibuni aliambatana na wadau mbalimbali wa Mahakama na kumtembelea Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel katika ofisi yake iliyopo kwenye jengo jipya la Makao Makuu ya Mahakama lililopo jijini Dodoma.
Jaji Ndika na wadau hao wa Mahakama wanakuwa miongoni mwa wageni wa awali kutembelea jengo hilo ikiwa ni siku chache tangu watumishi wa Mahakama kuanza kuhamia rasmi Dodoma. Wageni hao wa Mtendaji Mkuu walipata fursa ya kutembelea sehemu mbalimbali za jengo hilo la Makao Makuu ya Mahakama pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi ya Majaji unaoendelea kutekelezwa kwa kasi katika eneo la Iyumbu.
Akizungumza wakati anatoa neno la ukaribisho kwa wageni hao, Prof. Ole Gabriel amemshukuru Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na viongozi wengine ndani ya Mhimili wa Mahakama kwa usimamizi thabiti ambao umewezesha mpango wa kuanza kuhamia katika Makao Makuu ya Mahakama kutekelezwa kama ilivyopangwa.
Mtendaji Mkuu alibainisha kuwa mradi huo wa ujenzi wa jengo lenye vifaa na vitendea kazi vya kisasa ambalo litakuwa la sita kwa ukubwa duniani baina ya majengo ya Makao Makuu ya Mahakama, utagharimu takribani shilingi bilioni 129 za Kitanzania hadi kukamilika kwake.
Tayari jengo hilo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania lililopo katika eneo la Tambukareli limeanza kutumika tangu tarehe 29 Disemba, 2022.
Prof. Ole Gabriel alibainisha pia kuwa ujenzi wa nyumba za Majaji utawezesha viongozi hao kuwa na makazi ya uhakika na ya kisasa pindi watakapohamia Dodoma.
Kwa upande wake, Jaji Ndika alimpongeza Jaji Mkuu wa Tanzania na Mtendaji Mkuu kwa kuwa chachu na mstari wa mbele katika kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kuwezesha Mahakama kuhamia Dodoma.
Mara baada ya kutembelea maeneo mbalimbali, Mhe. Ndika alisifu uzuri wa kipekee wa jengo hilo, hivyo anaamini sehemu hiyo itakuwa kama motisha kwa watumishi kufanya kazi katika mazingira mazuri. “Sehemu nzuri na salama kwa kazi ni motisha kwa watumishi, motisha siyo fedha pekee” alisema Jaji Ndika.
Naye Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Fatmah Khalfan aliwapongeza viongozi wa Mahakama kwa hatua hiyo ya kuanza kuhamia Dodoma sambamba na kuipongeza Serikali kwa uwezeshaji wa ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama ya kisasa.