SERIKALI YATOA MAGARI MATANO NA KOMPYUTA MPAKATO 180 KWA TAASISI ZA UTOAJI HAKI
Na Selina Mlelwa, Tume ya Utumishi wa Mahakama
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Katiba na Sheria imetoa magari matano na kompyuta mpakato 180 kwa Mahakama ya Tanzania na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ili kuimarisha shughuli za utoaji haki nchini.
Wizara ya Katiba na Sheria imetoa magari matano na kompyuta Mpakato 30 kwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora pamoja na Kompyuta Mpakato 150 kwa Mahakama ya Tanzania.
Vifaa hivyo vimekabidhiwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Juma Homera (Mb), ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendeleza matumizi ya TEHAMA na kuimarisha utoaji haki nchini. Makabidhiano hayo yamefanyika tarehe15 Aprili, 2026 katika Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mgeni Rasmi, Mhe. Dkt. Homera alisema tukio hilo linadhihirisha dhamira ya dhati ya Serikali ya kuendelea kuimarisha sekta ya sheria ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wananchi wote kwa wakati na bila ubaguzi wa aina yoyote.
Alisema Serikali chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeweka kipaumbele katika kuboresha mazingira ya utendaji kazi kwa kuhimiza kutumia fursa iliyopo ya maendeleo ya TEHAMA ili kuimarisha mifumo ya utoaji huduma kwa Umma kwa njia ya kielektroniki.
“Maendeleo ya TEHAMA yaliyopo ni kichocheo kikuu cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Hivyo, kwa upande wa sekta ya sheria, matumizi ya TEHAMA siyo hiari tena, bali ni hitaji la msingi katika kujenga mfumo wa haki unaokwenda sambamba na mahitaji ya karne ya 21,” alisema Mhe. Dkt. Homera.
Kwa upande wake, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya akizungumza kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. George Masaju alisema vifaa walivyopokea vitasaidia kurahisisha usajili wa mashauri, usimamizi wa kumbukumbu na uendeshaji wa mashauri kwa njia ya mtandao (Video Conference) na kupunguza msongamano wa mashauri mahakamani.
Alisema vifaa hivyo pia vitawawezesha wananchi kupata huduma za Mahakama kwa urahisi zaidi bila kulazimika kufika mahakamani hasa kufungua mashauri, kufanya malipo na kufuatilia mwenendo wa mashauri yao.
Kupitia makabidhiano hayo, Tume ya Utumishi wa Mahakama ambacho ni chombo cha Usimamizi wa Uendeshaji wa Mahakama ya Tanzania itanufaika kwa kuwa Mhimili wa Mahakama utaongeza ufanisi katika utendaji kazi na kuboresha huduma za kimahakama hususan harakisha utoaji haki kwa wananchi.
Tume ya Utumishi wa Mahakama ni chombo kilichoanzishwa kwa mujibu wa Ibara ya 112 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, ikisomwa pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Mahakama, Sura ya 237 kwa lengo la kusimamia uendeshaji wa Mahakama ya Tanzania.
Aidha, Ibara ya 113 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ikisomwa pamoja na kifungu cha 29 (1) cha Sheria ya Usimamizi wa Mahakama sura ya 237 kinaipa Tume ya Utumishi wa Mahakama mamlaka ya kusimamia ajira na nidhamu za Watumishi wa Mahakama.

