MAHAKAMA ITAENDELEA KUIMARISHA UWAZI NA UWAJIBIKAJI:JAJI KIONGOZI


Na Lydia Churi- Tume ya Utumishi wa Mahakama- Arusha

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Mustapher Siyani amesema Mahakama itaendelea kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma zake.

Akifunga mafunzo yaliyolenga kuwajengea uwezo wakufunzi wa Kamati za Maadili za Maafisa Mahakama za Mikoa na Wilaya ambao ni Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Jaji Siyani amesema uwazi na uwajibikaji ni mambo yatakayosaidia kujenga imani ya wananchi kwa Mhimili wa Mahakama.

”Umma unayo haki si tu ya kusikia hatua zinazochukuliwa dhidi ya vitendo visivyokuwa vya kimaadili dhidi ya Maafisa Mahakama bali pia kuona namna hatua hizo zinavyochukuliwa”, alisema Kamishna huyo wa Tume.

Alisema ni matarajio ya Tume ya Utumishi wa Mahakama na Mahakama kuwa, elimu waliyopatiwa Majaji hao itakuwa ni chachu katika kuongeza uwajibikaji na utendaji kazo wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama za Mikoa na wilaya.   

Jaji Kiongozi aliwakumbusha Majaji umuhimu wa kujenga na kusimamia maadili ya Maafisa Mahakama na watumishi wengine wa Mahakama kwa kuwa kazi ya Mahakimu ni lazima iendane na maadili ndani yake.

”Maadili kwa Maafisa Mahakama ni chemchemi ya ustawi wa haki, uadilifu kwa Mahakimu na Majaji huzaa imani kwa wananchi, hakuna haki bila imani na hakuna imani bila uadilifu”, alisema.  

Alisema Kamati za Maadili zilianzishwa ili kuhakikisha Maafisa Mahakama wanatimiza wajibu wao kwa uadilifu na endapo kamati hizo hazitafanya kazi ipasavyo jamii itapoteza imani kwa Mhimili wa Mahakama.

Aliongeza kuwa kutoaminika kwa Mahakama kutasababisha hukumu zinazotolewa kutoheshimika na hivyo wananchi hawataona umuhimu wa kutumia Mahakama kama chombo rasmi kilichokasimiwa mamlaka ya kutoa haki.

Alisema Majaji wanayo kazi na wajibu wa kuendelea kuimarisha usimamizi wa maadili kupitia vyombo mbalimbali zikiwemo kamati za Maadili za mikoa na wilaya.

Alitoa wito kwa Majaji hao kutoa ushirikiano unaostahili kwa kamati za maadili zinapotekeleza majukumu yake kila inapohitajika kwani kutotimiza wajibu kwa kamati hizo ndani ya muda uliowekwa kunaweza kuzikwamisha kamati hizo kutekeleza jukumu lake la kusimamia maadili ya Maafisa Mahakama.   

Tume ya Utumishi wa Mahakama iliandaa mafunzo ya siku mbili kwa Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kutoka maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kuwajengea uwezo Majaji hao kwenda kutoa mafunzo yanayofanana (equal standard) kwa Wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama za Mkoa na Wilaya katika mikoa yote nchini.

Tume ya Utumishi wa Mahakama ni chombo cha kikatiba kilichopewa jukumu la kusimamia uendeshaji wa Mahakama ya Tanzania. Moja ya jukumu lake ni   kusimamia Maadili ya Maafisa Mahakama ili kuhakikisha Mhimili wa Mahakama unatekeleza jukumu lake la msingi na la kikatiba la kutoa haki kwa wananchi.

Jukumu la kusimamia maadili ya Maafisa Mahakama pamoja na majukumu mengine ya Tume, yameainishwa katika Ibara ya 113 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kifungu 29 cha Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Na.4 ya mwaka 2011.